Wednesday, October 17, 2012

Dk. Mwakyembe awataka Watanzania kuchangia elimu

WAZIRI wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, amewataka Watanzania kujenga utamaduni wa kuchangia elimu, kama wanavyofanya katika harusi. Kauli hiyo aliitoa Dar es Salaam jana wakati wa Mahafali ya Darasa la Saba na Shule ya Awali ya Shule ya Mwalimu Nyerere.

Alisema imekuwa jambo la kawaida kwa sasa, kukuta kundi la watu wamekaa kujadili michango ya harusi na kuacha elimu.

“Jamani mimi nimetembea sijaona mambo yanavyofanyika hapa Tanzania, majirani zetu tu hapo Kenya wanatushinda, Kenya hukuti watu wanachangisha harusi, kule ukikuta watu wamekaa ujue wanajadili suala la elimu.

“Hapa kwetu masuala haya ya harusi yanazidi kushamiri, zamani tulikuwa tunaona wasichana ndiyo wanafanyiwa kitchen party, lakini eti sasa hivi wanaume nao wanafanyia sijui begi party. Itafika mahali watu wataanzisha kaptula party.

“Watanzania tumeacha kabisa kuchangia elimu, tunaona harambee muhimu ni harusi, hebu tubadilike ndugu zangu, ukiona jirani yako au ndugu yako anashindwa kusomesha mtoto msaidie,” alisema Dk. Mwakyembe.

Aidha, alitoa wito kwa wanafunzi wa kike, kutokimbilia ndoa za utotoni na badala yake waweke juhudi katika masomo.

“Nawaasa wanangu wote, lakini zaidi ninyi wa kike ogopeni ndoa za utotoni, wekeni juhudi katika masomo mpate shahada nyingi zaidi, kwa kuwa sasa hivi tuko katika Jumuiya ya Afrika Mashariki na ushindani wa ajira utakuwa mkubwa,” alisema Dk. Mwakyembe.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Shule ya Mwalimu Nyerere, Jenerali Ulimwengu, alisema shule hiyo imeweza kukua kwa haraka toka wanafunzi 32 ilipoanzishwa hadi sasa ina zaidi ya wanafunzi 1,000, ambapo wanafunzi 127 wamehitimu darasa la saba kwa mwaka huu.

0 comments:

Post a Comment